TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI JUU
YA SIRI NZITO YA KIFO CHA MCHUNGAJI CHRISTOPHER REUBEN MTIKILA
Ndugu Wana-Habari,
Kabla sijawaeleza
kilichonilazimisha kuwaomba kuongea nanyinyi, kwanza niwarudishe nyuma kama
miaka saba iliyopita, ndipo maisha ya Baba, Mchungaji, Mwenyekiti na mume
wangu, Mchungaji Christopher Reuben Mtikila yalipoanzwa kuwindwa:-
MAUWAJI YA MHESHIMIWA CHACHA
ZAKAYO WANGWE
Mara tu baada ya kifo cha mbunge
huyo, mchungaji Mtikila alitoa ripoti maalumu juu ya mauaji yake ambayo
ilimjengea uadui kati ya baadhi ya vyama vya siasa pamoja na wafanyabiashara
wakubwa ambao hadi leo ni wapinzani wa serikali hapa
nchini. Mchungaji Mtikila hadi anafikwa na mauti aliendelea kupata
upinzani wa aina hiyo hiyo kwa sababu mchungaji Mtikila aliendelea kudai haki
ya marehemu Chacha Zakayo Wangwe.
MAUAJI YA BULIGI
Hii ilimwongezea uadui baada ya
kusema/kuandika ukweli juu ya watutsi wa nchi jirani kuvamia nchi yetu kwa
mtindo wa kujifanya wafugaji wasio hama. L.I.F. ilibaini uharamia huo kuwa
hawakuwa wafugaji bali walikuwa askari wa Jeshi la Rwanda waliokuwa na mpango
wa kutumika na Chama kimoja cha siasa hapa nchini ili kuleta mapigano yatakayo
zaa mapinduzi. Jambo hili lilisababisha Rais wa Rwanda, Paulo Kagame kutamka
hadharani kuwa angemkamata Mwenyekiti wa chama chetu cha DP kwa
lengo la kumuua na Serikali yetu inajua hilo. Mara baada ya ripoti hiyo kutolewa
na Mchungaji Mtikila "operation Kimbunga" ilizaliwa na kuponya nchi
yetu; lakini chuki na uadui uliendelea dhidi ya Mchungaji Mtikila.
MCHAKATO WA URAIS NDANI YA CCM
Ikumbukwe kuwa mara baada ya
mchakato wa kutafuta mgombea urais kwa tiketi ya CCM kuanza DP ilitoa ripoti
iliyowahusu wagombea sita wa CCM waliotumia mapesa mengi na kuanza kampeni
kabla ya muda na kusisitiza kuwa Lowasa ni mtu asiefaa kuwa Rais wa nchi yetu.
Na baada ya kuhama CCM, Mwenyekiti wetu aliendelea kutoa tahadhari hadharani
jinsi Lowasa asivyofaa kuwa Rais wa nchi yetu hivyo likaendeleza uadui wake na
Chama.
VITISHO KUANZA
Mchungaji Mtikila alipata nafasi
ya kuongea katika kipindi kinachorushwa na STAR TV cha asubuhi
"TUONGEE" ndipo alipoanza kupata vitisho toka kwa watu mbali mbali wengine
kupitia kwenye simu wengine uso kwa uso. Kipindi cha kwanza kilirushwa tarehe
25/9/2015 na kufuatwa na cha tarehe 27/9/2015. Alipotoka studio hiyo asubuhi ya
tarehe 27/9/2015 ndipo watu waliodai wametumwa na Mhe. Edward Ngoyai Lowasa na
Mhe Frederick Sumaye walimuomba wampe nusu bilioni na apewe maovu ya mgombea
urais wa CCM ili afunike alivyowamaliza wao. Mchungaji Mtikila aliwapuuzia
mbali wale wajumbe waliyotumwa kwni aliawaambia kuwa yeye siyo malaya wa kuuza
utu wake kwa tende na haluwa. Yakumbukwe kuwa mahojiano kwenye hivyo vipindi
viwili kwenye STAR TV hayakuwa yanatetea mtu au chama yalikuwa yanatetea Taifa
letu lipate Rais anayefaa. Kwa hiyo basi wale waliochukizwa na mahojiano hayo
ni wale amabo hawakubaliani na mawaidha ya Mchungaji Mikila aliyokuwa
anawatahadharisha watanzania juu ya Mh. Lowasa kuwa hatari kwa usalama wa taifa
letu kama atakuwa Rais wa nchi yetu. Hao watu ndiyo waliopanga mpango mzima wa
mauaji ya Mh. Mtikila ambaye ni mume wangu. Wakati yuko Bunda mjini watu
wasiofahamika walimfuatafuata na tarehe 26/9/2015 gari lake lilifukuzwa na gari
usiku wakati alipokuwa anatoka Bunda kwenda Mwanza kufanya mahojiano ya tarehe
27/9/2015 na Star Tv.
MPANGO WA MAUAJI HALISI
Mchungaji Mtikila alitafutiwa gari
na Victor James Manyahi ambayo ilikuwa na madereva wawili. Mchungaji madereva
hakuwajua. Hata mimi madereva hao sikuwajua wala sikuwaona. Walikodiwa kutoka
wapi sijui, wala sijui wanafanana vipi. Na wala sijui Victor Manyahi alikodi
gari hilo kwa nani na makubaliano yepi sijui. Kwa hivyo basi, kwenye gari
aliyosafiri nayo Mchungaji Mtikila kulikuwamo madereva wawili na Mgaya Patrick
(tunayemfahamu). Wakati wanakwenda gari lilipata ajali Makambako. Wakati
wanarudi wakapata “ajali” Msolwa Mchungaji akapatwa na mauti peke yake. Ajali ilikuwa
mbaya sana IKAUWA MTU MMOJA AMBAYE NI MCHUNGAJI MTIKILA NA HAKUKUWA
MAJELUHI HATA MMOJA. Cha ajabu kwangu n kuwa mtu ambaye alikuwa ni mlinzi
wa kujitolea (body guard) Mgaya Patrick sijawahi kumuona usoni mwangu kabla na
hata baada ya mazishi kuja kuniambia kilichotokea eneo la ajali. Pamoja na
juhudi zangu zote za kumpigia simu mara kadhaa aje anijuze Mgaya Patrick
hajatokea hadi sasa ndugu zangu wanahabari ninapoongea nanyi. Lakini si kwamba
huyu mtu hayupo, yupo lakini sijaonana naye, kwa nini sijui. Je ndugu zangu
wanahabari nimuweke Mgaya Patrick kwenye fungu gani?
Ndugu Wana-Habari, baada ya
kuwaelezea yote hapo juu nakuja kwenye suala nililowaomba nikutane nanyi ili
niongee mbele yenu kuwa sikubaliani na uchunguzi kuwa Mchungaji Christopher Reuben
Mtikila amekufa kwa ajali. Sikubaliani na kazi ya Polisi kuwa wamefunga file
lao kutokana na Post-mortem report kuwa mauti yaliotokana na ajali. Nafuta
kabisa taarifa iliyotoka katika gazeti la Nipashe chini ya kichwa
cha habari kuwa “FAMILIA YAFUNGUKA KIFO CHA MTIKILA”-ilitolewa mapema mno. Kila
mwanafamilia alikuwa hajawa tayari kutoa kauli yoyote. Kwa niaba ya Chama na
familia ya Mchungaji Christopher Reuben Mtikila naomba tusaidiwe yafuatayo
kusudi haki ya mpendwa wetu ionekane inatendeka:-
Kwa sababu mtandao umeanza kuficha
ukweli ili kulinda wauaji; tunaomba Mheshimiwa Rais aingilie utata wa kifo cha
Mheshimiwa Mchungaji Christopher Reuben Mtikila kwa kuunda tume ya uchunguzi
isiyohusisha polisi.Tunaiomba mamlaka ya mawasiliano yaani Tanzania Communications
Regulatory Authority, TCRA itusaidie yafuatayo:-
(a) Mtu
aliyeweka picha kwanza alfajiri kuonyesha mauti ya Mhe Mchungaji Mtikila
alikuwa wapi? Kwenye tukio? Au ni hao wauaji walikuwa wanatoa taarifa kwa
waajiri wao kuwa wamekamilisha kazi!
(b) Mtu
aliyeweka picha ya Dr. Jean-Bosco Ngendahimana kwenye mtandao kuwa ndiye
anahusika na mauti ya Mhe. Mch. Mtikila na kumusingizia kuwa amekamatwa na
polisi akiwa anajiandaa kukimbia;
(c) Wote
wanaoendelea kumhusisha Dr. Jean-Bosco Ngendahimana na mauaji ya Mhe. Mchungaji
Mtikila, tuwafahamu ili watueleze vizuri.
Ukweli na haki ni vya Mungu hakuna
anayeweza kuviua au kuvizuia. Tunategemea Mungu atawatumia watendaji wa
Serikali/nchi yetu wenye nia njema, na makusudi yaliyonyooka kwa ajili ya nchi
yetu ili Mhe. Mchungaji Mtikila apewe haki dhidi ya wauaji wake.
Asanteni,
No comments:
Post a Comment