Social Icons

Friday 9 May 2014

LEO KATIKA MAHUSIANO: USIKUBALI KUACHIKA UKIWA KWENYE UCHUMBA, KAMA UMECHUMBIWA NA HAELEWEKI INGIA HAPA FASTA UJIFUNZE


UJANA una mambo mengi lakini vijana wa zama hizi tumezidisha. Matukio ndani ya uhusiano ni mengi zaidi ya wakati uliopita. Kukutana na wanandoa wanaoachana baada ya miaka miwili tu ni jambo la kawaida siku hizi.

Si ajabu tena kusikia msichana amechumbiwa na amevalishwa pete kabisa lakini baada ya siku kadhaa anaachwa. Hii ni aibu! Utakuta msichana hadi anaingia kwenye ndoa, ameshavaa pete za uchumba kutoka kwa wanaume hata wanne tofauti!

Ni mabadiliko mabaya lakini yanayosababishwa na mfumo mpya wa maisha ya sasa. Ndugu zangu, lazima tujifunze mambo muhimu ya kufanya ili uhusiano uwe wenye maana.

Vilio vya wasichana wengi ni kuhusu kuvalishwa pete au kudumu kwenye uchumba kwa muda mrefu, lakini ghafla mwanaume anamuacha na kuanzisha uhusiano na mwingine.

Hebu tujiulize; ni tamaa za wanaume hao au tatizo lipo kwa wanawake wenyewe? Dada zangu, naomba mfahamu kuwa, wakati mwingine ninyi ndiyo husababisha matatizo na hatimaye kuachwa.
Je, nini cha kufanya? Hapa nitakupa mambo muhimu ya kukaa nayo mbali ili uweze kuingia kwenye hatua inayofuata – ndoa. Karibuni darasani.

KAA MBALI NA WANAUME
Wapo ambao wamejikuta wakiachwa solemba kufuatia tabia zao za kuwa na mazoea ya kijinga na wanaume.

Yawezekana kabla ya kuchumbiwa, marafiki zako wakubwa walikuwa wanaume (Wapo wanawake wa aina hiyo).

Unachotakiwa kufahamu ni kwamba hakuna mwanaume anayefurahia ukaribu wa mchumba wake kwa wanaume wengine.

Hata kama hakuna uhusiano wa kimapenzi lakini epuka sana kujichekelesha kwao, kuongozana nao, kukaa nao au hata kuwasiliana nao. Ukifanya hivyo utakuwa unamkwaza mchumba wako na inaweza kuwa moja ya sababu za kukuchenga.

CHAGUA MARAFIKI
Kipindi cha uchumba ni wakati ambao msichana anatakiwa kuwa makini sana na marafiki, akae mbali na wale mapepe!

Nazungumzia wale micharuko ambao hawawezi kukushauri vizuri juu ya maisha yako. Hata wale ambao wamekuwa wakikushawishi kila wikiendi muende mkajirushe, baada ya kuchumbiwa unatakiwa kujiweka mbali nao ili kumpa amani mchumba wako.

PUNGUZA USICHANA
Ukishachumbiwa wewe si msichana tena, utakuwa ni mama mtarajiwa wa familia yako. Tabia za kisichana kama vile kuvaa mavazi yasiyo ya heshima, kukaa vijiweni kuongea mambo ya umbeya na nyinginezo kama hizo hutakiwi kuendelea kuwa nazo.

USIHAMIE KWAKE
Hili baadhi ya wanaume wanapenda sana lakini kwa usalama wa msichana si jambo zuri.
Kuolewa ni mpaka pale mtakapoingia kanisani, msikitini, kwa viongozi wa kiserikali nk na kufungishwa ndoa.

Kama bado hamjafika huko, wewe bado ni mchumba tu na hata kwenye ndoa unaweza usifike.
Kwa maana hiyo hutakiwi kuhamia kwa mwanaume kama ambavyo baadhi wamekuwa wakifanya.
Unachotakiwa kufahamu ni kwamba kitendo cha wewe kuchumbiwa kisha kuamua kubeba virago vyako na kwenda kuishi na mwanaume ni kuwakosea wazazi wako.

Ukiachwa itakuwa aibu ya nani? Jibu unalo. Hadi wiki ijayo kwa mada nyingine, USIKOSE!
Joseph Shaluwa ni Mshauri wa Saikolojia ya Uhusiano anayeandikia Magazeti ya Global Publishers. Kwa sasa anaandaa kitabu chake kipya cha Maisha ya Ndoa.

GPL

No comments: