Social Icons

Monday 7 May 2012

LEO KATIKA MAHUSIANO: UKITAKA SALAMA KWENYE MAPENZI, USIFANYE MAKOSA HAYA


NI matumaini yangu kuwa wasomaji wangu muwazima bukheri wa afya. Ni wiki nyingine tena tunapokutana katika uga wa mahaba, na kujuzana mambo kadha wa kadha yahusuyo uhusiano wa kimapenzi. Leo tunaendelea na mada yetu ya namna ya kuyaepuka makosa yanayoweza kukukosesha amani katika uhusiano wako. Twende pamoja...

Kama hakuvutii achana naye mapema, usimpotezee muda wako. Muda wako pia ni mali, kwa hiyo hilo pia litazame kwa umakini kwa sababui inawezekana ukachukulia ni jambo dogo leo, ukaanza naye uhusiano kwa kujifurahisha lakini mbele ya safari utakapotaka kuamua, ikakugharimu kwa maana pengine wakati wewe unawaza kutoka, mwenzako ndiyo kwanza anaongeza gia.
4) Kipimo cha mapenzi: Hiki ni kipengele nyeti. Kina maana kubwa, kwa hiyo hupaswi kudanganyika kwa namna yoyote ile. Hakikisha upendo wake kwako upo wazi. Wengi hushindwa kulifanyia kazi mapema, matokeo yake hubaki wakijuta baadaye. Chukua angalizo hili, kwa hiyo kama haoneshi upendo wa kweli, vema umuache aende.
Je, anaonesha yupo tayari kwa ujenzi wa uhusiano imara? Yupo wazi kwako na anapenda kila mtu ajue kwamba yeye ni wako? Alama hizo ndizo ambazo zinaweza kukupa muongozo unaojitosheleza. Kama upendo wake ni wa wasiwasi, nawe mkatae haraka. Wekeza upendo kwenye upendo, vinginevyo wewe utampenda lakini mwenzako atakudharau.
KUAMUA UHUSIKA WAKE KWENYE UHUSIANO
Ni rahisi kuamua jinsi ambavyo wewe unavyoweza kuhusika kwenye uhusiano wako lakini si yeye. Kufanya hivyo ni sawa na kuingia kwenye moyo wa mwingine, kitu ambacho hakiwezekani hata kiduchu. Kaa ukijua kwamba nafsi ya kwanza itabaki kuwa ya kwanza na ya pili itaendelea kusimama katika uhalisia wake.
Maisha ni kama picha ambayo unaijenga kwenye fikra zako. Endapo utawaza mema na kutamani kumfanyia mwenzi wako vitu vizuri, ni rahisi kutekeleza. Utakosea mno, kama utakuwa unasumbuliwa na mawazo kwamba unachokitenda, mpenzi wako naye atakaa na kufikiria kisha akutendee kama unavyomfanyia.
Kwa miaka kadhaa, nimejifunza kujua tabia za watu kwenye mapenzi na kubwa ambalo nimebaini ni kwamba saikolojia ya ndani ndiyo ambayo inaleta utata. Uhusiano wa wengi unashindwa kudumu kwa sababu hiyo. Ukweli ni kwamba ndani ya mtu, kunakuwa na matarajio ambayo hayafikiriwi upande wa pili.
Hili ni tatizo lakini linaweza kuwa kinyume chake kama mhusika ataligundua hilo na kulitafutia ufumbuzi. Kwa nini uwaze peke yako? Iweje kichwa kiume kwa tamaa ya kutekelezewa jambo ambalo linaweza kuingizwa kwenye majadiliano? Mapenzi ni kitu kinachokutanisha nafsi mbili zenye hisia tofauti, kwa hiyo inabidi kuelewana ili muende sawa.
Acha kuwaza peke yako. Mshirikishe mwenzako jinsi ambavyo wewe ungefurahi kwa namna atakavyohusika kwenye mapenzi yenu. Muelekeze cha kufanya. Mshauri muonekano ambao wewe utakupa nguvu ya kujiamini kwamba upo kwenye uhusiano salama. Usipojadiliana naye, unadhani utasaidiwa na nani?
Kosa kubwa ambalo watu wengi huwa wanafanya ni kuwaacha wapenzi wao na kwenda kujadiliana na marafiki. Mtu anaweza kuketi na rafiki yake na kummwagia lawama chungu nzima jinsi asivyofurahishwa na mwenzi wake, wakati angezungumza na mhusika mafanikio yangeonekana kwa urahisi zaidi.
Achana na tabia ya kumsengenya mwenzi wako kwa marafiki zako. Unamponda kwa yale anayofanya kwa kuona hayapo sawa lakini mapenzi hayapo hivyo. Tambua kwamba wewe pekee ndiye mwenye nafasi ya kumfanya mpenzi wako abadilike kulingana na jinsi unavyotaka. Jijengee mawazo chanya kuanzia leo.
Binadamu walivyo katika jinsi mbili tofauti, ndivyo wanavyotofautishwa na namna ya kupenda pia jinsi ya kuhusika kwenye mapenzi.
Itaendelea wiki ijayo.

www.globalpublishers.info

No comments: