Social Icons

Friday 24 August 2012

LEO KATIKA MAHUSIANO: KUACHWA KUPO TU, MUDA UKIFIKA HUNA SABABU YA KUUMIA!



WIKI hii mpenzi msomaji wangu nataka kuzungumzia hii ishu ya wapenzi kutosana. Katika ulimwengu wa sasa tumekuwa tukishuhudia wapenzi waliotokea kupendana sana wakiachana tena wakati mwingine katika mazingira yasiofaa.
Hilo si la kushangaa kwani limekuwepo tangu enzi za mababu zetu, walipendana lakini pia wapo waliokuwa wakiachana kwa mateke na mangumi.

Haya hivyo, kuachwa ukusikie hivihivi kwa wenzako, inauma sana pale unapomkosa mtu ambaye huenda ulishaamini atakuwa wako wa maisha. Maumivu ya kuachwa ndiyo yanayowafanya baadhi ya watu kufikia hatua ya kuchanganyikiwa na wengine kunywa sumu.
Ndiyo maana wataalam wa masuala ya mapenzi wanasema, usiombe ukaachwa. Bora ukishaona dalili ya kuachwa ukawahi kuacha wewe ili angalau kujipunguzia maumivu.
Kutokana na mzingira hayo, unashauriwa unapoingia kwenye uhusiano wa kimapenzi na mtu uliyetokea kumpenda, usimkabidhi moyo wako kwa asilimia zote.
Chukua muda wa kumchunguza ili kubaini kama na yeye pia anakupenda kwa dhati kutoka moyoni mwake. Ukishabaini hili, nawe mkabidhi moyo wako kisha myafurahie maisha yenu.
Lakini ukiona moyo wako unasita kuendelea kuwa na mtu huyo na kuhisi hana penzi la kweli, ni vizuri bila kujali jinsi utakavyoumia ukamuacha haraka kabla ya yeye hajakupiga chini.
Kumuacha kwako kutakufanya uwe na amani moyoni, kwani utakuwa umejiandaa kumkosa kuliko yeye kuamua kukuacha ghafla, utaumia sana!
Nalazimika kuandika makala haya kwa kuwa, unamkuta mtu anaumizwa kila wakati na mpenzi wake lakini kwa sababu tu anampenda, anaamua kuvumilia huku akiamini ipo siku penzi lao litatengemaa.
Hutakiwi kulilea penzi lisilokuwa na muelekeo, usikubali kulizwa, unapoona nyendo za mpenzi wako hazikuridhishi, chukua uamuzi wa haraka wa kumuacha.
Kimsingi mtu asiye na penzi la kweli, utamgundua tu. Kwa mfano mpenzi wako anakuwa mgumu wa kuonana na wewe, mawasiliano duni, msiri sana, hakujali, kumpenda kwako anaona kama unajipendkeza, haoni hatari kukueleza kwamba muachane, haoneshi kukupenda kiivyo, huyu ipo siku atakuacha na kukumiza sana.
Sasa kwa nini usichukue hatua za haraka za kuwahi kumtosa? Kuna raha gani ya kuwa na uhusiano na mtu asiyekupa raha ya maisha?
Usikubali kuwa mtumwa wa mapenzi kwa kukubali kuburuzwa na mtu unayeweza kumuacha na maisha yako yakaendelea kuwepo. Amini wewe ni mzuri, ‘handsome’ na una kila kigezo cha kupata penzi la uhakika na si la kubabaisha.
Wapo ambao wamekuwa wagumu kuwaacha wapenzi wao kwa maelezo kwamba, bila wao maisha yao hayawezi kukamilika. Hebu jiulize, kabla ya kuwa naye huyo uliye naye hukuwa na maisha? Maisha yako hayawezi kukamilika bila yeye kwani mlizaliwa pamoja?
Ifike wakati ujiangalie wewe kama wewe. Ujione mwenye nafasi ya kuishi maisha ambayo unayataka wewe, namaanisha maisha ya furaha ambayo utayapa ukiwa na mtu anayekupenda na kukupa amani ndani ya moyo wako.
Utakuwa ni mtu usiyejali maisha yako kama utamganda mtu ambaye unaona wazi hana dhamira nzuri na wewe. Kumbuka wapo watu ambao waliishi na wapenzi wao kwa muda mrefu sana lakini baadaye waliamua kuwaacha baada ya kubaini walijiingiza sehemu isiyo sahihi
Kitu kizuri ni kwamba, ukiwaangalia sasa wanaishi kwa amani baada ya kuwapata wale walio na mapenzi ya dhati kwao. Sasa inakuwaje kwako wewe ambaye uko kwenye penzi lisilo na nyuma wala mbele hadi leo?
Unajiuliza utayaepukaje maumivu ya kumkosa mtu uliyekuwa umemkabidhi moyo wako?
Amini huyo siye uliyepangiwa na Mungu
Kila binadamu ameshapangiwa maisha yake ya hapa ulimwenguni. Ameshapangiwa mtu wake wa kuishi naye kama mke na mume na ameshapangiwa staili ya maisha yake. Ukiona huyo uliyenaye anakuletea za kuleta, elewa kuwa huyo siye uliyepangiwa naye.
Kaa utulie huku ukiamini kuwa wako yuko njiani na muda si mrefu utakuwa naye na kuyafurahi maisha yako.

www.globalpublishers.info

No comments: