Social Icons

Tuesday 18 June 2013

LEO KATIKA MAHUSIANO: UTAMU AU MATESO YA MAPENZI HUTOKANA NA MTINDO WAKO WA MAISHA


Dhana ya mtu kuonekana wa kiwango cha chini (mara nyingi kujiona yeye mwenyewe) kwenye mapenzi, niliichambua wiki iliyopita. Ukweli ni kwamba kuna njia nyingi ambazo zinaweza kukufanya ujione dhalili kwenye uhusiano wako;
mathalan, pale unapowasilisha hisia zako za kweli jinsi unavyompenda mwenzi wako. Hapo ni lazima uwe umejishusha, kwani unakuwa umemuweka juu mwenzi wako kwamba yeye ana thamani kubwa kwenye maisha yako.
Fikiria kuwa unamwambia kuwa yeye ni kila kitu kwako. Hapo unakuwa umejishusha sana na kumdhihirishia kuwa bila yeye maisha yako yatakuwa na pengo kubwa. Ikiwa mwenzi wako ni mwelewa, naye atatafuta neno lenye thamani inayokaribiana na hilo kisha atakwamba. Mfano; atakwambia wewe ni dunia yake.
Mapenzi ni sanaa nzuri sana. Haihitaji mtu wa nje kuweza kuwaunganisha. Nyoyo zinapokuwa zinakubaliana, fedha hukosa nafasi kabisa. Huboreshwa na hisia zinazoingia na kutoka, yaani kila mmoja awe na mguso wa hisia za mwenzake. Kwa kifupi, mapenzi bora ni yale yanayojengwa na hisia za kubadiliashana (give and take).
Usione shida kabisa. Kubali kujishusha kadiri inavyowezekana. Pengine ukawa unajiona dhalili pale unapoelezea namna ulivyo au mapito yako ya nyuma. Unaweza kujihisi mnyonge unapokuwa unakiri kosa. Usikubali kiburi kikutawale, usipende mamlaka kwa mwenzi wako. Yeye ajishushe, nawe jishushe, utaona uhusiano wenu utakavyokuwa bora.
Nguvu na mamlaka vinavyokutawala, hukufanya ushindwe kujidhibiti. Unaweza kumtamkia mwenzo wako neno lolote. Kujishusha, hukusababishia wewe kujiongezea sifa na uhalali wa kuitwa mpenzi. Yaheshimu mapenzi, maana yakikunyookea na maisha huwa bora pia. Ukiogopa kuwa mnyonge, ukataka uonekane upo juu, mapenzi kwako yatageuka mateso.

8. FIKIRI KABLA HUJAFANYIA KAZI HISIA
Unapoongozwa na hisia, utajikuta unafanya makosa mengi kila siku. Fikiria kuwa kuna kitu kinakunong’oneza kuhusu ubaya wa mwenzi wako. Kila baada ya muda, kitu hicho kinakukumbusha ndani kwa ndani. Kama hutakuwa makini, unaweza kujikuta unafanya uamuzi wa kijinga ambao kwako baadaye utakusababishia mateso.
Hisia chanya siku zote zinatokana na mguso wa Mungu, hisia hasi huchagizwa na ushawishi wa Shetani. Hivyo basi, unaweza kumhukumu mwenzi wako kwa sababu hisia zako zimekutuma. Hisia hasi ni kichocheo cha jazba, kwa hiyo kuwa mwangalifu sana juu ya hilo, unaweza kujizulia aibu.
Fikiria kwamba kuna kitu kinakunong’oneza kwamba mwenzi wako ana mtu mwingine. Hilo linapokushika sawasawa ni majanga, kwani unapompigia simu akichelewa kupokea, moja kwa moja utahisi yupo anafanya mambo mabaya. Akichelewa kujibu SMS, utawaza yupo kona anachakachua penzi lako.
Akikujibu SMS kwa kifupi kutokana na kutingwa na kazi, kichwani kwako utaona ni kiburi kwa sababu anaye mtu mwingine. Kwa kifupi ni janga zito sana kubeba hisia hasi na kuishi nazo. Hebu fanyia kazi katika kuzitokomeza, vinginevyo zinaweza kukuendesha na kukufanya ufanye vitu kwa kukurupuka.
Nyongeza ya hapo ni kwamba hofu na hisia hasi ni vitu vinavyoendana. Mara nyingi ni lazima uwe na hofu ndipo utaanza kumhisi vibaya mwenzi wako. Haiwezekani ukawa huhofii kitu halafu uwe unamhisi tofauti. Siku zote shindana na hofu kwenye mapenzi, wengi zimewapeleka nje ya mstari.
Kwa kawaida, hofu hutokana na kukosekana kwa uaminifu. Anza kumwamini mwenzi wako kisha uone matunda yake. Utakuja kubaini kwamba huna hofu hata kidogo. Vivyo hivyo, utajigundua hakuna hisia yoyote mbaya juu ya mwenzi wako ambayo inapita kwenye fikra zako.
Kuna kitu ambacho mara nyingi huwa kigumu. Kudhibiti hisia. Kila mmoja huhitaji utatuzi wa haraka hususan pale anapokuwa na hasira. Pengine kuna SMS ambayo haieleweki, ameiona kwenye simu ya mwenzi wake. Wengi wetu hukimbilia kuwasha moto badala ya kuketi pamoja na kusaka ufumbuzi.
Hebu jiwekee utaratibu wa kupenda kusikiliza kutoka kwa mwenzi wako kabla ya kuamka ukiwa mbogo na kuanza kushusha maneno mazito ukimtuhumu mwenzi wako. Fanya mazoezi ya kuufunga moyo wako kwanza ili upate nafasi ya kumsikiliza mwenzi wako, usikie anakwambia nini.
Pengine katika maelezo yake ukapata suluhu itakayokuweka mbali na maumivu ya moyo kuliko hatua ambazo utazichukua kutokana na kuongozwa na jazba. Umeona SMS ya mapenzi kweye simu ya mwenzi wako kutoka kwa mtu mwingine, huwezi kujua kama iliingia kwa bahati mbaya kama hutataka kusikiliza.
Ni kazi sana kusikiliza wakati umeona kitu unachoweza kukilinganisha na ukweli. Hata hivyo, nakusihi ufanyie mazoezi suala la kuufunga moyo. Kwa maana moyo unaweza kukupeleka kwenye uamuzi wa haraka, ukatoa hukumu ambayo siyo. Siku ukijua kama ulimhukumu mwenzi wako kimakosa, utaumia sana.
Ni ukweli kwamba kila mmoja wetu anapojisikia kuumia, lazima apatwe na hali ya hasira na kuchanganyikiwa. Ni hapo ndipo hutaka kufanya kitu cha kujiweka salama na wakati huohuo kumbomoa yule ambaye unadhani amekutenda. Hebu fanyia kazi hilo, hisia zisikuongoze. Kila hisia, ifanyie kazi kwanza.CHANZO: GPL

No comments: