Social Icons

Friday 27 September 2013

KUSALITIWA, KUACHWA NI KUBAYA, YAKUPASA KUWAJIBIKA KAMA MWANAMKE.. SOMA HAPA


Tunakutana tena kupitia ukurasa huu ambao ni namba moja kwa kuandika makala nzuri zinazogusa maisha yako ya kimapenzi. Ukiwa unaufuatilia kila wiki, mapenzi hayawezi kukutesa kama yanavyowatesa wengine.

Utajua mbinu bora za kumpata mwenza sahihi lakini pia jinsi ya kuishi naye kwa raha mustarehe na kamwe asifikirie kukusaliti wala kukuacha. Mpenzi msomaji wangu, leo nataka kuzungumza na wanawake walio kwenye ndoa lakini pia si vibaya na wale wanaotarajia kuingia kwenye maisha hayo wakasoma.

Ndugu zangu, vilio vya baadhi ya wanawake kuibiwa waume zao na kuachwa vimekuwa vikiongezeka kila kukicha lakini nimebaini kitu kimoja. Wengi wanakutwa na janga hili kwa kushindwa kutimiza wajibu wao kama wanawake, wanalilia kuolewa na wakibahatika kuingia kwenye maisha hayo wanajisahau na kubweteka.

Kimsingi mwanamke anayemjali mpenzi wake ndiye anayetimiza wajibu wake, lakini wengi hujikuta wakitoswa na wapenzi wao kutokana na ufahamu mdogo ama dharau ya mambo madogomadogo.

Ni busara kutambua kuwa uhusiano hauna mambo ‘simpo’. Kila kitu kina umuhimu mkubwa kulingana na nafasi yake sambamba na utekelezaji wako.

Mwanaume hata siku moja harogwi kwa limbwata la sangoma, mahaba yaliyoshiba peke yake yanatosha kumfanya awe hapindui kwako. ‘Ukimhendo’ kwa kiwango kitakachomridhisha, hatowaza kukuacha. Unawezaje? Jibu ni rahisi, muoneshe unampenda na thibitisha kwa vitendo.

Daima hili liwe akilini mwako, mwanamke kupitia mapenzi yake ana uwezo mkubwa mno, lakini lazima awe anajua kutimiza wajibu wake kwenye uhusiano.

Kama mpenzi wako anakuacha, ujue kuwa umeshindwa kuchukua nafasi yako kama mwanamke na kuna mambo unayomkosea. Unyenyekevu kwa wanawake wa kisasa kimekuwa ni kitu adimu, kiasi ambacho kinahatarisha uhusiano wa watu wengi.

Wanaume wanawapenda wanawake ambao hujionesha waziwazi kuwa wenyewe ni wasaidizi wao wakuu katika masuala mbalimbali hivyo anza leo kutimiza wajibu wako.

Hii ni moja ya mbinu za kumdatisha mwenzi wako na ninachotaka ukijue ni kwamba, wengi wamefanikiwa na ndiyo hao ambao leo hii wanazifurahia ndoa zao na kujihisi wako peponi.

Lakini kitu kingine ambacho nahisi unatakiwa kukijua ni kwamba, mke wa mtu au mwanamke yeyote aliye kwenye uhusiano anatakiwa kuwa mjanja. Hii ni kwa sababu wanaume wengi wanapenda kuwa na watu wa dizaini hii.

Sababu ya wanaume kuwapenda wanawake wajanja ni kukwepa aibu wanazoweza kuzipata pindi watakapokuwa kwenye uhusiano na washamba.

Wanaume wengi huogopa kujiingiza katika mapenzi na watu wasiokuwa na uelewa mpana wa mambo ambao kutokana na tongotongo za ufahamu, hujikuta wakiwa mafundi wa kuiga mambo ya hatari.

Washamba mara nyingi huwa ni malimbukeni, hujifunza mambo yasiyokuwa na faida kwa imani kwamba naye ataonekana mtu kati ya watu. Wanawake wa aina hii ni rahisi kuwaingiza wenzi wao katika hasara kubwa. Hawakawii kuiba, ni rahisi kuharibu vitu, wao ni wabadhilifu na wanaopenda makuu! Wanawake malimbukeni huharibika katika vikao vya ususi, kutokana na sifa kubwa ya umbeya kwenye sehemu hizo. Wanaume wasiokuwa na subira hujikuta wakiwapiga teke wenzi wao mara tu wanapoanza kuhisi nyendo zisizoeleweka.

Tumekuwa tukishuhudia wanawake malimbukeni wakiiga tabia za ulevi wa pombe au mihadarati kutoka kwa marafiki zao. Wengine hubadilika na kufikia hatua ya kuwa mafuska waliokubuhu huku wakiwapanga mabwana kila kona.

Mwanamke mjanja hawezi kuiga hovyo hovyo, siku zote anajua kitu cha kuanzia na kinachofuata. Hawadanganyiki kwa penzi la pesa, wanaelewa malipo yake ni makubwa. Ndiyo maana wanaume wanawapenda!

Nawe kama unataka kupendwa zaidi kuwa mjanja, lakini zaidi ya yote chukua nafasi yako kama mwanamke kisha timiza wajibu wako. Majibu yake utayaona.

CHANZO GLOBAL PUBLISHERS

No comments: