Hivi karibuni kumejitokeza uzushi unaosambazwa katika
mitandao ya kijamii ya ndani ya nchi na nje ya nchi kuwa Rais wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli amefukuza wageni
kutoka nje waliokuwa wanafanyabiashara zao nchini kwa kuwa serikali yake
haitaki wageni kufanya biashara nchini.
Serikali haijafukuza wageni kutoka nje ya nchi kufanya
biashara nchini na haina mpango wa kuwafukuza wageni wanaoishi nchini kwa
vibali vilivyotolewa kisheria na Idara ya Uhamiaji.
Uzushi huo usiokuwa na ukweli umeenezwa kufuatia Idara
ya Uhamiaji kutekeleza jukumu lake la kufuatilia wageni wote wanaoishi nchini
bila vibali halali vya ukaazi ambapo kwa mwezi Novemba na Desemba mwaka 2015
wageni 372 walioondoshwa nchini.
Kazi ya kufuatilia wageni wanaoishi nchini bila vibali
halali vya kisheria haijaanza katika Serikali ya Awamu ya Tano. Idara ya
Uhamiaji nchini tangu Januari hadi Desemba mwaka jana iliondosha nchini jumla
ya wageni 1,642 waliokuwa wanaishi na kufanya shughuli zao nchini kinyume na
Sheria.
Uzushi unaoenezwa hauna ukweli wowote na hauna nia
njema na nchi yetu kwani kati ya mwaka 2014 na 2016 Idara ya Uhamiaji imetoa
vibali vya ukaazi (Residence Permits) 40,765 kwa wageni wawekezaji na
wafanyabiashara, wageni wanaofanyakazi za kuajiriwa, wageni wanaokuja kwa ajili
ya Masomo, matibabu, dini, utafiti na wastaafu kuishi na kufanya shughuli zao
nchini.
Serikali
inawakaribisha wageni kuja nchini kuwekeza na kufanya shughuli zao kwa kufuata
Sheria, Kanuni na Taratibu za nchi.
Aidha,
kuna uzushi unaenezwa kuwa Rais Dkt John Pombe Magufuli amepiga marufuku
wanawake kuvaa nguo fupi kama njia ya kupunguza kasi ya maambukizi ya ugonjwa
wa UKIMWI.
Mheshimiwa
Rais tangu aingie madarakani hajawahi kuagiza wala kutoa tamko kuhusiana na
uzushi wa kukataza uvaaji wa nguo fupi ili kupunguza maambukizi ya Ukimwi kama
inavyoenezwa katika mitandao ya ndani na Nje ya Nchi ambayo inanukuu habari
hiyo kuwa imeandikwa na Gazeti la Kenya “The Standard”
Serikali
inapenda kuutangazia umma kuwa uzushi huo unaomhusu Mheshimiwa Rais Magufuli
umetungwa na watu wasioitakia mema nchi yetu kwa lengo la kumdhalilisha Rais na
hauna ukweli hivyo watu wasishiriki kuueneza kwa njia yeyote ile.
Serikali
kupitia balozi zake za Kenya na Afrika Kusini zinafuatilia chanzo cha uzushi
huu kuhusu Rais Magufuli kwa kushirikiana na nchi husika na watakaobainika
kutunga na kueneza uzushi huu watachukuliwa hatua za kisheria.
No comments:
Post a Comment