Mke wa Rais wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mama Janeth Magufuli aliyekuwa amelazwa katika
wodi ya Sewahaji ya Hospitali ya Taifa Muhimbili Jijini Dar es Salaam
ameruhusiwa na kurejea nyumbani leo tarehe 11 Novemba, 2016 baada ya afya yake
kuimarika.
Kabla ya kuondoka
katika wodi ya Sewahaji alikokuwa amelazwa Mama Janeth Magufuli amewashukuru
Madaktari na Wauguzi wa Hospitali ya Taifa Muhimbili kwa matibabu mazuri
aliyoyapata na pia amewashukuru Watanzania wote kwa kumuombea afya njema.
"Namshukuru
sana Mungu kwamba afya yangu imeimarika, pia napenda kuwashukuru Madaktari na
Wauguzi, nimepata huduma nzuri sana maana siku nilipoletwa hapa nilikuwa sina
fahamu na hali yangu ilikuwa mbaya lakini mmenipigania na leo narudi nyumbani
nikiwa na afya imara.
"Naomba pia
niwashukuru Watanzania wote kwa kuniombea, nawahakikishie kuwa sasa nipo vizuri
na madaktari wameniruhusu nirudi nyumbani ambako nitamalizia matibabu
yangu" amesema Mama Janeth Magufuli.
Mama Janeth
Magufuli alilazwa hospitalini hapo tangu Juzi tarehe 09 Novemba, 2016 baada ya
kuugua ghafla na kupoteza fahamu.
Gerson
Msigwa
Mkurugenzi
wa Mawasiliano ya Rais, IKULU
Dar es
Salaam
11 Novemba,
2016
No comments:
Post a Comment