Social Icons

Tuesday 24 April 2012

Twanga yamnyakua mpiga tumba Mapacha Watatu



Na Mwandishi Wetu
BENDI ya muziki wa dansi ya African Stars 'Twanga Pepeta' imemnyakua
mpiga tumba wa bendi ya Mapacha Watatu, Salehe Waziri maarufu kama
'Salehe Tumba' kuziba pengo la Said Mohammed 'MCD' aliyetimkia Mashujaa.



Akizungumza na Jambo Leo, Dar es Salaam jana, Mkurugenzi wa African
Stars Entertainment Tanzania (ASET) inayomiliki bendi ya Twanga Pepeta,
Asha Baraka, alisema hatua ya kumnyakua mpiga tumba huyo ni kuimarisha
bendi yake.



" Tayari tumekwishakamilisha taratibu za makubaliano na  mwanamuziki
huyo na tumesaini naye mkataba wa miaka mitatu leo (jana)," alisema
Baraka.



Alisema Waziri ataungana na Badi Bakule aliyejiunga na bendi hiyo hivi
karibuni akitokea Levent Musica ya Morogoro, na akawaomba mashabiki wa
bendi yake wakae mkao wa kuendelea kupata burudani safi kutoka kwa bendi
hiyo ambayo ni 'kisima cha burudani'.



Mkurugenzi huyo alisema Waziri aliyewahi kupigia bendi dada ya zamani ya
Twanga Pepeta, Chipolopolo, ataungana na mpiga tumba mwingine, Kaboshoo
huku akishirikiana na wapiga vyombo wengine, Miraji Shakashia
'Shakazulu', James Kibosho, Jumanne Mkandu 'Jojoo', Godfrey Kanuti,
Victor Mkambi na Selemani Shaibu.



Pia anaungana na wanenguaji, Abdillahi Zungu, Kassim Mohammed 'Super K',
Bakari Kisongo 'Mandela' Said Mtanga, Fasha Sunday, Beatrice Mwangosi
'Baby Tall', Asha Said 'Sharapova', Mary Khamis, Vicky Pandapanda,
Sabrina Mathew na Maria Soloma.



Baadhi  ya waimbaji ni Saleh Kupaza, Mwinjuma Muumini, Ramadhani
Athumani 'Dogo Rama', Luiza Mbutu, Msafiri Said 'Diouf', Jumanne Said,
Khamis Amigolas, Venance Mgori, Haji Ramadhan, Hadija Mnoga 'Kimobitel',
Janeth Isinika.



Alisema hivi sasa wanajiandaa kuingia studio kwa ajili ya kurekodi wimbo
wao mpya wa Shamba la Twanga uliotungwa na Grayson Semsekwa na pia
kurekodi video za wimbo huo na nyingine mpya.

No comments: