Ikiwa unataka tengenezewa Blog, Tukiko lolote la Harusi,Msiba, Mahafali, Tamasha, Matangazo auHabari yoyote usisite kututumia kupitia whatsapp 0765056399 au Barua Pepe fredynjeje@live.com. Follow me instagram @fredynjejeblog Twitter @Fredynjeje
Waziri
wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais, January Makamba amesema uwajibikaji
katika utawala wa Serikali ya Awamu ya Nne haukuwa wa kuridhisha kwa
sababu kulikuwa na utamaduni wa kuoneana haya, kujuana, kusitiriana na
kutoogopa.
Amesema
hayo yalikuwa yakitokea kwa kuwa waliokuwa wakifanya makosa hawakuwa
wakichukuliwa hatua na hivyo kujengeka utamaduni wa watu kutoogopa,
lakini sasa utawala mpya umeonyesha kuchukua hatua dhidi bila ya woga.
Makamba,
ambaye aliingia tano bora ya mbio za urais ndani ya CCM kabla ya
kuangushwa kwenye kikao cha Halmashauri Kuu, alitoa kauli hiyo juzi
katika mahojiano maalumu na Mwananchi ofisini kwake jijini Dar es Salaam
juzi.
Alikuwa
akijibu swali kuhusu hatua ambazo zimekuwa zikichukuliwa na Serikali ya
Rais John Magufuli dhidi ya wakwepa kodi, wabadhirifu, watendaji
wazembe na wezi wa mali za umma, tofauti na utawala uliopita wa Serikali
ya Awamu ya Nne.
“Nadhani
moja ya changamoto zilizosababisha huko nyuma tusifanikiwe sana katika
suala la uwajibikaji, ni hili suala la kuoneana haya. Ni hili suala la
kuweka kujuana kidogo na ni hili suala la kusitiriana,” alisema Makamba,
ambaye alikuwa Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia
kwenye utawala uliopita.
“Na ukijengeka huo utamaduni na ukajikita mizizi, hatua hazitakuwa zinachukuliwa dhidi ya watu wanaofanya makosa.”
Udhaifu
katika kuchukulia hatua watumishi wanaofanya makosa ulikuwa kilio
kikubwa cha wanasiasa dhidi ya utawala uliopita na wakati fulani katibu
mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana aliwahi kusema kuwa Serikali ni dhaifu
kwa kuwa inasitasita katika kuchukua uamuzi.
Wakati
fulani, mbunge wa Ubungo (kabla ya jimbo kugawanywa), John Mnyika
alikwenda mbali zaidi na kusema kiongozi wa Serikali ndiye dhaifu kwa
kuwa Katiba inampa haki ya kutosikiliza ushauri wa mtu wala chombo
chochote iwapo ataona hivyo.
Utumbuaji majipu
Lakini
tangu Novemba 5, 2015 wakati Magufuli alipoapishwa, takribani watumishi
160 wa Serikali wameshasimamishwa kazi au uteuzi wao kutenguliwa
kutokana na kutuhumiwa kuhusika katika ubadhirifu wa fedha za umma,
kufanikisha ukwepaji kodi, uzembe na wizi.
“Kwa
hiyo kila kiongozi ana staili yake ya namna ya kufanya, lakini mimi
kimsingi—kwa sababu hizi kazi ni za umma si kazi zetu binafsi—kimsingi
sioni tatizo watu kuambiana ukweli na kama mtu anadhani kwamba ameonewa
basi fursa zipo za kutafuta haki yake kutokana na hayo ambayo anadhani
kwamba hayajakaa vizuri.
“Kikubwa
tu ambacho mimi naamini kinafanyika na kilihitajika ni kujenga
utamaduni mpya wa watu kuogopa na kuheshimu wajibu wao, na kwamba hizi
kazi si kazi zetu za kudumu. Wakati wowote unapofanya makosa basi kuna
mamlaka ya kukuchukulia hatua. Na kwamba kule nyuma ambako watu hawakuwa
wanaogopa kabisa, huo si utamaduni ambao kwa kweli ulikuwa unafaa
katika kujenga taifa jipya.”
Akizungumzia
lawama kuwa staili hiyo ya kutumbua majipu inafanywa kwa kuumbua watu
na kwamba makosa hayo yalishafanyika tangu utawala uliopita bila
kuchukuliwa hatua, Makamba alisema kosa linapobainika wakati wowote
lazima lichukuliwe hatua.
“Kama
huko nyuma hakukuwa na utashi wala mifumo ya kuwezesha makosa hayo
kubainika, lakini utashi huo upo sasa, basi hatua zichukuliwe,” alisema
Makamba ambaye ni mtoto wa aliyekuwa Katibu Mkuu wa CCM, Yusuph Makamba.
“Kila
kiongozi ana staili yake na Rais Magufuli amekuja na ujasiri na anataka
kujenga nidhamu mpya kwenye nchi,” alisema Makamba.
“Hana
deni na mtu. Hii ni falsafa na dira ambayo kiongozi anataka nchi iende
kulingana na anavyotaka kuitengeneza. Ni jambo jema kwa sisi
tunaomsaidia serikalini na ndani ya CCM.”
Akizungumzia
hatua za kuwasimamisha kazi watendaji kwa tuhuma mbalimbali, alisema
urais ni taasisi na kwamba kiongozi huyo wa nchi anapotoa amri ya
kukamatwa au kufukuzwa kwa mtendaji hakurupuki.
“Nyuma
yake kuna mfumo uliomsaidia kuchukua uamuzi huo. Wanaochukuliwa hatua,
sheria, kanuni na taratibu za utumishi wa umma zinakuwa zimefuatwa,”
alisema.
Kuhusu
watendaji kusimamishwa kazi ndani ya vikao au katika ziara za mawaziri,
huku baadhi wakiwa wamefanya makosa hayo miaka mitano iliyopita,
Makamba alisema: “Sidhani kama kuna ukomo wa uharamu wa kosa, kwamba kwa
sababu ulifanya kosa mwaka 2012 likibainika mwaka 2015 si kosa tena.
Mantiki hii sikubaliani nayo.”
Alisema mtu aliyefanya kosa miaka mitano iliyopita, likibainika sasa na ushahidi ukapatikana lazima achukuliwe hatua.
Bomoabomoa
Kuhusu
utekelezaji wa kubomoa nyumba zilizojengwa mabondeni, Makamba alisema
utaratibu huo ulikuwepo katika awamu zote nne zilizopita, lakini tatizo
sheria za utekelezaji wake hazikuwa zikifuatwa kikamilifu.
“Bonde
la Msimbazi lilitangazwa kuwa eneo hatarishi kwa maisha ya watu tangu
mwaka 1949 na baadaye mwaka 1979. Kumekuwa na taratibu za kuondoa watu
ili kurejesha maeneo hayo katika hali ya yake ya asili,” alisema.
Alisema
Wizara ya Ardhi na Maendeleo ya Makazi iliwahi kutangaza Bonde la
Msimbazi kuwa eneo maalum ma mipango miji, ili kutimiza suala hilo
ilikuwa lazima watu waondolewe.
Alisema
kazi ya kuwaondoa wananchi wanaoishi kwenye bonde hilo ilikumbwa na
changamoto kadhaa na kukajengeka dhana kuwa wanaonewa.
“Serikali
tulieleza kama mtu alipewa kibali na Serikali akajenga nyumba, basi
Serikali ilifanya makosa na itamtafutia mahali pengine. Ila kama mtu
alikuja tu na kujenga nyumba eneo hilo lazima aondoke,” alisema Makamba.
Alisema
waliovamia mabondeni na kujenga, Serikali haiwezi kuweka utaratibu wa
kuwapatia maeneo mengine kwa sababu kufanya hivyo ni sawa sawa na kuwapa
zawadi wanaovunja sheria.
Alisema
licha watu hao kujenga nyumba zao mpaka kufikia hatua ya kuanza kuishi,
haiwezi kuwa kipimo cha kujipambanua kuwa hawana makosa.
“Unapofanya
makosa ukamilifu wa kosa siyo msamaha kwa kutorekebishwa. Ukisema kwa
sababu mtu hakukamatwa wakati akijenga msingi, basi asikamatwe kwa
sababu nyumba imeisha si kweli,” alisema.
Alisema
kazi ya kubomoa nyumba zilizopo mabondeni iliingiliwa na wanasiasa na
akasisitiza kuwa maisha wanayoishi wananchi katika maeneo hayo, si ya
kuridhisha na ukiwa kiongozi huwezi kukubali kuona wakiendelea kuishi
humo.
“Sisi
ambacho tumekubali lazima tuliendeshe zoezi lile kwa utaratibu mzuri
zaidi. Lazima watu wapate taarifa na waliovamia kuelezwa wazi kuwa
hawatapata stahiki yoyote na waliopewa vibali na Serikali wapewe maeneo
mengine,” alisema Makamba.
“Kuna
utamaduni ulijengeka kwa muda mrefu wa watu kutoheshimu na kutii
sheria. Sasa tukiendelea hivyo hivyo si sawa maana bila sheria hakuna
Serikali. Nchi hii mtu hawezi kuamua kujenga kibanda popote na
akiondolewa Serikali ndiyo ionekane ina dhambi. Hatuwezi kuendesha nchi
kwa utaratibu huu.”
Lakini Makamba alikanusha kwamba Serikali ilitekeleza ubomoaji huo kwa kuwa ilishajihakikishia ushindi kwenye Uchaguzi Mkuu.
“Niseme
zoezi hili ni endelevu na limeanza kabla ya Serikali kuingia
madarakani. Ila pia nyakati za kufanya maamuzi mazito ni nyakati za
mwanzo za utawala mpya,” alisema.
“Magufuli
ni Rais anayependa sheria za nchi zifuatwe na utekelezaji wa sheria
hizo usilete mzozo na vurugu. Tumekaa na kukubaliana namna nzuri ya
kufanya jambo hili. Walioenda mahakamani tutasubiri maana zuio la
mahakama linahusu sehemu tu ya eneo si bonde zima. Kwingine tunakoweza
kufanya tutaendelea.”
MWANANCHI
No comments:
Post a Comment