Ikiwa unataka tengenezewa Blog, Tukiko lolote la Harusi,Msiba, Mahafali, Tamasha, Matangazo auHabari yoyote usisite kututumia kupitia whatsapp 0765056399 au Barua Pepe fredynjeje@live.com. Follow me instagram @fredynjejeblog Twitter @Fredynjeje
P.O. Box 8031, Dar es
Salaam, Tel: 2110585, 2122771/3, Fax:
2113814, e-mail: maelezo@habari.go.tz Tarehe: 01/03/2016
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
Gazeti la Dira ya Mtanzania, Toleo
Na.404 la Februari, 29 – Machi 6, 2016 liliandika taarifa yenye kichwa cha
habari kisemacho “Uchafu wa Ombeni Sefue
Ikulu”. Taarifa hiyo, ambayo ni muendelezo wa makala nyingine
kwenye toleo la gazeti hilo la wiki iliyopita, ilimtuhumu Katibu Mkuu Kiongozi
kushawishi juu ya uteuzi wa Mkurugenzi Mkuu wa MSD pamoja na Kampuni za “CRJE” na “UGG” kupewa tenda ya kujenga Chuo Kikuu cha Dodoma, Daraja la
Kigamboni na Reli ya Dar es Salaam - Kigali. Taarifa zote hizi ni za uongo na
za kupotosha wananchi.
Kuhusu uteuzi wa nafasi ya Mkurugenzi Mkuu wa MSD,
Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Ombeni Sefue, hakuhusika kwa namna yoyote kushawishi uteuzi
wa Mkurugenzi Mkuu wa MSD. Uteuzi huo ulitekelezwa kwa kufuata kanuni na
taratibu zilizowekwa. Nafasi hiyo ilitangazwa na Bodi tarehe 20 Novemba, 2013.
Usaili ulifanywa na kampuni huru iliyopewa jukumu hilo na Bodi. Mapendekezo ya
majina matatu yalipelekwa kwa Mhe. Rais na Waziri wa Afya, kwa ajili ya uteuzi.
Balozi Sefue alikuwa hamjui
aliyeteuliwa na wala hakuwahi kuwa na uhusiano naye. Alichofanya Balozi Sefue ni kutangaza tu uteuzi
baada ya Rais kuteua. Gazeti hilo pia limeandika uwongo kuwa MSD haijawahi
kuongozwa na Mkurugenzi Mkuu asiye Mfamasia.
Tangu MSD ianzishwe mwaka 1993 hadi sasa, ni Mkurugenzi Mkuu mmoja tu,
Rino Meyers (1996-1999), ndiye alikuwa Mfamasia.
Wakurugenzi wengine kama Peter Mellon
(1993-1995), Jay Drosin (2001-2004) na Joseph Mgaya (2004-2013) hawakuwa
Wafamasia.
Kuhusu Kampuni ya CRJE kuhusishwa na Balozi Ombeni Y.
Sefue
Suala la kumhusisha Katibu Mkuu Kiongozi na kampuni
hii nalo ni uzushi na uongo wa kupindukia. Wakati kampuni hii ikipewa tenda ya kujenga
Chuo Kikuu cha Dodoma mwezi Oktoba 2007, Balozi
Ombeni Y. Sefue hakuwa Katibu Mkuu Kiongozi; alikuwa Balozi wa Tanzania
nchini Marekani. Kadhalika mchakato wa kumpata mkandarasi wa daraja la Kigamboni,
ulipoanza mwezi Machi, 2011, Balozi Sefue
hakuwa Katibu Mkuu Kiongozi; alikuwa Balozi wa Tanzania, Umoja wa Mataifa, New
York. Hata mkataba wa ujenzi wa Daraja hilo uliposainiwa tarehe 9 Januari, 2012, Balozi
Sefue alikuwa na wiki moja tu ya kuwa Katibu Mkuu Kiongozi kufuatia kuteuliwa
tarehe 30 Disemba, 2011. Aidha, Kampuni iliyoshinda tenda hiyo wala siyo
CRJE kama ilivyoandikwa na gazeti hilo bali ni China Major Bridges Engineering
Company (BCEC) kwa kushirikiana na Kampuni ya China Railway Construction
(CRCEG).
Kuhusu tuhuma kuwa Katibu Mkuu Kiongozi Chapuo Kampuni
ya UGG:
Katibu Mkuu Kiongozi hajawahi kuipigia chapuo kampuni
yoyote ile pahala popote. Isitoshe, hakuna kampuni yenye jina la “UGG”
iliyowahi kuonesha nia ya kujenga reli ya kati. Hii ni moja ya uthibitisho
kwamba gazeti hili linatoa taarifa za
kuokoteza zisizo na ukweli kama vile walivyopotosha kuhusu jina la Katibu Mkuu
Kiongozi kwenye makala yao ya pili kwenye ukurasa wa tisa wa gazeti hilo yenye
kichwa cha habari “Magufuli anaishi na
jipu Ikulu” ambapo walimpachika Katibu Mkuu Kiongozi jina la Sifuni, jina ambalo hajawahi kuwa nalo. Balozi
Sefue hajahusika, hahusiki na wala hatahusika katika kuchagua wa kupewa
tenda hiyo kwa sababu yeye si sehemu ya wenye mamlaka ya kutoa tenda.
Kuhusu Eliachim Maswi:
Gazeti
la Dira ya Mtanzania limeandika kuwa moja ya “madudu” aliyofanya Balozi Sefue ni walichoita kumsafisha Bwana
Eliachim Maswi. Wanadai hivyo
wakati wamekiri kuwa alichofanya Balozi
Sefue ni kusoma matokeo ya uchunguzi, ambao hakuufanya yeye. Waliomsafisha Maswi ni Mdhibiti na
Mkaguzi Mkuu wa Serikali; Sekretarieti ya Maadili ya Umma; na hatimaye kamati
ya uchunguzi iliyoongozwa na Jaji wa Mahakama Kuu. Kwa hiyo, kwa maoni ya gazeti hili, Balozi Sefue asingepaswa kusoma matokeo
ya uchunguzi uliofanywa na vyombo hivyo huru.
Kwa maoni yao
kusoma taarifa ya uchunguzi ni “madudu”.
Habari hizo hazina chembe yoyote ya ukweli, na wao
wenyewe ndani ya gazeti wamekiri hawana ushahidi, ni wazi kuwa habari hizo ni za kubuni na
zimetungwa.
Kwa sababu hiyo, Serikali inalitaka Gazeti la Dira ya
Mtanzania kukanusha uongo na uzushi wao na kumuomba radhi Balozi Ombeni Sefue, kuiomba radhi Serikali na kuwaomba radhi wote
walioumizwa na uzushi huo kwa uzito ule ule uliotumika kuchapisha
taarifa hiyo.
Vinginevyo iwapo gazeti la Dira ya Mtanzania lina
ushahidi wa huo “uchafu” wa Katibu Mkuu Kiongozi, waupeleke mara moja kwenye vyombo
vinavyohusika ikiwamo Sekretarieti ya Maadili na TAKUKURU. Vinginevyo,
hatua zikichukuliwa dhidi yao wasiseme Serikali inavibana vyombo vya habari.
Aidha Serikali inashauri
wenye vyombo vya habari, wachapishaji, wahariri na waandishi wa habari wajikite
kwenye weledi na ukweli, wafanye utafiti na kuandika mambo waliyo na uhakika
nayo, na kamwe wasikubali kutumiwa kuendeleza agenda za watu wengine.
No comments:
Post a Comment