Social Icons

Monday 27 March 2017

DKT ABBASI: MAAFISA HABARI HARAKISHENI KUTOA TAARIFA ZA SERIKALI KWA UMMA

Ikiwa unataka tengenezewa Blog, Tukiko lolote la Harusi,Msiba, Mahafali, Tamasha, Matangazo au Habari yoyote usisite kututumia kupitia whatsapp 0765056399 au Barua Pepe fredynjeje@live.com. Follow me instagram @fredynjejephotography Twitter @Fredynjeje





Na Mwandishi Wetu
Dodoma
MAAFISA Habari na Mawasiliano Serikalini wametakiwa kutoa taarifa kwa haraka zaidi kwa kutumia njia za kisasa za mawasiliano ikiwemo tovuti na mitandao ya kijamii ili kusaidia kutangaza Mafanikio ya Serikali katika maeneo yao ya kazi.

Hayo yamesemwa jana Mkoani Dodoma na Mkurugenzi wa Idara ya Habari (MAELEZO) na Msemaji Mkuu wa Serikali Dkt. Hassan Abbasi, alipokuwa akizungumza na maafisa habari na TEHAMA katika mafunzo elekezi ya uwekaji wa taarifa katika tovuti yanayofadhiliwa na Shirika la Misaada la Marekani (USAID) na kusimamiwa na Ofisi ya Rais- TAMISEMI na Wakala ya Serikali Mtandao (EGA).
Dkt. Abbas alisema kuwa mara baada ya tovuti kuzinduliwa rasmi, Maafisa Habari wana wajibu wa kuweka taarifa mpya zinazozingatia muda na wakati kwa kuwa malengo ya tovuti hizo ni kumsaidia mwananchi kuweza kupata taarifa mbalimbali za Serikali.
“Tukifungua tovuti hizi tunapaswa kuona taarifa mpya, kwa sasa suala la upashanaji wa habari na taarifa za miradi ya  Serikali isisubiri tena michakato, isipokuwa kama kutatokea suala kubwa ambalo litahitaji ufafanuzi kutoka katika ngazi za juu katika maeneo yenu ya kazi” alisema Dkt. Abbasi
Aliongeza kuwa, taaluma ya habari katika zama za sasa inahitaji ubunifu mkubwa katika kuisemea Serikali kwa kutafuta njia mbalimbali za kubaharisha umma badala ya kutumia njia za kawaida na za kila siku.
“Katika maeneo yetu ya kazi tuna vituo vya redio na televisheni ambazo zinawahitaji Viongozi wetu kufanya nao mahojiano maalum kuhusu masuala mbalimbali ya Serikali, ni wajibu wetu kutumia fursa hizo kuhakikisha tunaisemea Serikali” alisema Dkt. Abbasi.
Kwa mujibu wa Dkt. Abbasi alisema Serikali itaweka utaratibu maalum wa kupima utendaji kazi wa kila Afisa Habari katika Wizara, Idara, Taasisi, Wakala na Mamlaka za Mikoa na Wilaya na Mikoa ili kuona ni namna gani ameweza kutoa taarifa za Serikali kuhusu masuala mbalimbali ya Serikali.
“Katika kipindi hiki Serikali ya Awamu ya tano imetekeleza na inatekeleza miradi mikubwa ya maendeleo ikiwemo miradi ya umeme vijijini (REA), na ujenzi wa miundombinu mingine kwa kutumia fedha nyingi katika kutekeleza miradi hiyo, hivyo ni wajibu wa Maafisa Habari kueleza wananchi utekelezaji wa miradi hiyo” alisema Dkt. Abbasi.
Alisema kuwa ili taarifa hizo za utekelezaji wa mafanikio hayo ya Serikali ziweze kuwafikia wananchi, ni wajibu wa Maafisa Habari na Mawasiliano kujenga na kuimarisha mtandao wa mawasiliano baina yao pamoja na  watendaji wengine katika maeneo yao ya kazi.
Aliongeza kuwa ubunifu ni siri nyingine ya mafanikio katika suala la upashanaji wa taarifa za Serikali, hivyo ni wajibu wa Maafisa Habari kuwa mbunifu badala ya kulalamika kutokana na changamoto mbalimbali zinazomkabili katika maeneo yao ya kazi ikiwemo ufinyu wa bajeti na changamoto ya ukosefu wa vitendea kazi.
Mafunzo hayo ya wiki moja yalishirikisha mikoa na Halmashauri za Mikoa ya Arusha, Manyara, Singida, Dar es salaam, Pwani na Dodoma.

No comments: