
Na Mwandishi Wetu
Dodoma
MAAFISA
 Habari na Mawasiliano Serikalini wametakiwa kutoa taarifa kwa haraka 
zaidi kwa kutumia njia za kisasa za mawasiliano ikiwemo tovuti na 
mitandao ya kijamii ili kusaidia kutangaza Mafanikio ya Serikali katika 
maeneo yao ya kazi.
Hayo
 yamesemwa jana Mkoani Dodoma na Mkurugenzi wa Idara ya Habari (MAELEZO)
 na Msemaji Mkuu wa Serikali Dkt. Hassan Abbasi, alipokuwa akizungumza 
na maafisa habari na TEHAMA katika mafunzo elekezi ya uwekaji wa taarifa
 katika tovuti yanayofadhiliwa na Shirika la Misaada la Marekani (USAID)
 na kusimamiwa na Ofisi ya Rais- TAMISEMI na Wakala ya Serikali Mtandao 
(EGA).
Dkt.
 Abbas alisema kuwa mara baada ya tovuti kuzinduliwa rasmi, Maafisa 
Habari wana wajibu wa kuweka taarifa mpya zinazozingatia muda na wakati 
kwa kuwa malengo ya tovuti hizo ni kumsaidia mwananchi kuweza kupata 
taarifa mbalimbali za Serikali.
“Tukifungua
 tovuti hizi tunapaswa kuona taarifa mpya, kwa sasa suala la upashanaji 
wa habari na taarifa za miradi ya  Serikali isisubiri tena michakato, 
isipokuwa kama kutatokea suala kubwa ambalo litahitaji ufafanuzi kutoka 
katika ngazi za juu katika maeneo yenu ya kazi” alisema Dkt. Abbasi 
Aliongeza
 kuwa, taaluma ya habari katika zama za sasa inahitaji ubunifu mkubwa 
katika kuisemea Serikali kwa kutafuta njia mbalimbali za kubaharisha 
umma badala ya kutumia njia za kawaida na za kila siku.
“Katika
 maeneo yetu ya kazi tuna vituo vya redio na televisheni ambazo 
zinawahitaji Viongozi wetu kufanya nao mahojiano maalum kuhusu masuala 
mbalimbali ya Serikali, ni wajibu wetu kutumia fursa hizo kuhakikisha 
tunaisemea Serikali” alisema Dkt. Abbasi.
Kwa
 mujibu wa Dkt. Abbasi alisema Serikali itaweka utaratibu maalum wa 
kupima utendaji kazi wa kila Afisa Habari katika Wizara, Idara, Taasisi,
 Wakala na Mamlaka za Mikoa na Wilaya na Mikoa ili kuona ni namna gani 
ameweza kutoa taarifa za Serikali kuhusu masuala mbalimbali ya Serikali.
“Katika
 kipindi hiki Serikali ya Awamu ya tano imetekeleza na inatekeleza 
miradi mikubwa ya maendeleo ikiwemo miradi ya umeme vijijini (REA), na 
ujenzi wa miundombinu mingine kwa kutumia fedha nyingi katika kutekeleza
 miradi hiyo, hivyo ni wajibu wa Maafisa Habari kueleza wananchi 
utekelezaji wa miradi hiyo” alisema Dkt. Abbasi.
Alisema
 kuwa ili taarifa hizo za utekelezaji wa mafanikio hayo ya Serikali 
ziweze kuwafikia wananchi, ni wajibu wa Maafisa Habari na Mawasiliano 
kujenga na kuimarisha mtandao wa mawasiliano baina yao pamoja na  
watendaji wengine katika maeneo yao ya kazi.
Aliongeza
 kuwa ubunifu ni siri nyingine ya mafanikio katika suala la upashanaji 
wa taarifa za Serikali, hivyo ni wajibu wa Maafisa Habari kuwa mbunifu 
badala ya kulalamika kutokana na changamoto mbalimbali zinazomkabili 
katika maeneo yao ya kazi ikiwemo ufinyu wa bajeti na changamoto ya 
ukosefu wa vitendea kazi.
Mafunzo
 hayo ya wiki moja yalishirikisha mikoa na Halmashauri za Mikoa ya 
Arusha, Manyara, Singida, Dar es salaam, Pwani na Dodoma.
No comments:
Post a Comment