Social Icons

Monday 18 September 2017

NMB IWASAIDIE WAFANYABIASHARA SINGIDA KUANZISHA KIWANDA CHA VIFUNGASHIO; DKT NCHIMBI


1
Mkuu wa Mkoa wa Singida Dkt Rehema Nchimbi akisalimiana na Mwenyekiti wa klabu ya wafanyabiashara wateja wa NMB Singida Emmanuel Rweyemamu Kyoma mapema leo kabla ya kufungua warsha ya siku moja ya klabu hiyo, katika ukumbi wa Kanisa Katoliki mjini Singida.


2
Mkuu wa Mkoa wa Singida Dkt Rehema Nchimbi akikagua baadhi ya bidhaa za wafanyabiashara wateja wa NMB Singida mapema leo kabla ya kufungua warsha ya siku moja, katika ukumbi wa Kanisa Katoliki mjini Singida.
3
Meneja wa NMB Kanda ya kati Straton Chilongola akizungumza klabu ya wafanyabiashara wateja wa NMB Singida mapema leo wakati wa ufunguzi wa warsha ya siku moja, katika ukumbi wa Kanisa Katoliki mjini Singida.
4
Wafanyabiashara wateja wa NMB Singida wakiwa katika warsha ya siku moja katika ukumbi wa Kanisa Katoliki mjini Singida mapema leo.
………………………………………………………………………
Benki ya NMB imetakiwa kuwasaidia wafanyabiashara Mkoani Singida kuanzisha kiwanda cha kutengenea vifungashio, ili waweze kuhifadhi bidhaa zao katika ubora unaokubalika kitaifa na kimataifa.
Mkuu wa Mkoa wa Singida Dkt Rehema Nchimbi ametoa rai hiyo mapema leo wakati akifungua warsha ya siku moja ya klabu ya wafanyabiashara wateja wa NMB, katika ukumbi wa Kanisa Katoliki mjini Singida.
Dkt Nchimbi amesema klabu hiyo ya wafanyabiashara itaweka alama kubwa katika maendeleo endapo watajipanga na kuanzisha kiwanda cha kutengeneza vifungashio hivyo kuliko kuendelea kuvifuata nje ya Singida au nje ya nchi.
“Uzoefu usipotumika vizuri unaweza ukawa kikwazo cha kuendelea, msizoee kufuata vifungashio na label nje ya singida wakati fursa ipo ya kuanzisha kiwanda hicho Singida”, amesema na kuongeza kuwa,
“Wafayabiashara mzipende biashara zenu na kuziweka katika hali ya usafi na yenye kuvutia, wengine wanapenda kujisafisha na kujipendezesha wenyewe lakini ukiangalia biashara zao hazivutii, zimewekwa tu bila kufungashwa vizuri”, amesisitiza.
Aidha amewataka wafanyabiashara wasiogope kukopa kwakuwa sio jambo la aibu wala fedheha, ila kinachotakiwa ni kuwa na nidhamu ya mkopo na malengo ili waweze kufanikiwa.
“Akina mama jifunzeni kuwa na nidhamu ya mkopo, sio unakopa leo mara unasikia kapu la mama, jifikirie hayo ndio malengo ya huo mkopo hata kama ni jambo muhimu?, nidhamu ya mkopo inatakiwa ianze kabla ya kukopa na iendelee kuwepo.
Dkt Nchimbi pia ameishukuru benki hiyo kwa kushirikiana na serikali katika mambo mbalimbali ya kielimu na afya, pia amewashukuru kwa kutoa mikopo kwa watumishi wa umma jambo ambalo linawasiadia katika mambo mbalimbali.
Naye Meneja wa NMB Kanda ya kati Straton Chilongola amesema klabu za wafanyabiashara nchini ziko 34 ambazo zimekuwa zikipatiwa mafunzo mikopo kutoka katika benki hiyo.
Chilongoloa amesema benki hiyo imekuwa ikitoa mafunzo juu ya ulipaji kodi, ujasiriamali, masuala ya mitaji, leseni na ardhi ili wafanyabiashara hao waweze kukuza mitaji yao.
Amesema benki hiyo imefanikiwa kuwakuza wafanyabiashara wengi ambazo wameanza nao wakiwa wafanyabiashara wadogo ambapo sasa wamekuwa wakubwa na wakati huku wakiajiri wengine na hivyo kukuza uchumi.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa klabu ya wafanyabiashara wateja wa NMB Singida Emmanuel Rweyemamu Kyoma amesema wazo la kuanzisha kiwanda cha kutengeza vifungashio wamelipokea vizuri huku wakijipanga kuandaa andiko kwa ajili ya kiwanda hicho.
Kyoma amesema kwa ushirikiano na NMB kiwanda hichokitaweza kujengwa Singida huku wakimuahidi Mkuu wa Mkoa kuwa Mkoa wa Singida utazalisha chakula cha kutosha kulisha Mkoa wa Dodoma.
Amesema benki ya NMB imekuwa ikishirikiana na wafanyabiashara hao hivyo mipango ya kukuza uchumi kama huo wa kuanzisha viwanda utatekelezeka bila matatizo yoyote.

No comments: