Social Icons

Wednesday 3 February 2016

HOTUBA YA MHESHIMIWA MAMA JANETH MAGUFULI, MKE WA RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA KWENYE KITUO CHA MAKAZI YA WAZEE NA WATU WALEMAVU WASIOJIWEZA NUNGE, KIGAMBONI, TAREHE 3 FEBRUARI, 2016

Ikiwa unataka tengenezewa Blog, Tukiko lolote la Harusi,Msiba, Mahafali, Tamasha, Matangazo auHabari yoyote usisite kututumia kupitia whatsapp 0765056399 au Barua Pepe fredynjeje@live.com. Follow me instagram @officialfredynjejeblog Twitter @Fredynjeje

Mke wa Rais Mama Janeth Magufuli akihutubia wakaazi wa  Kituo cha Makazi ya Wazee na Watu Walemavu cha Nunge, Kigambo ni, jijini Dar es salaam alikotembelea na kusikiliza mahitaji yao pamoja na kutoa msaada wa mchele kilo 3000, Unga kilo 3000 na Maharage Kilo 1200 ikiwa msaada wake kwa wazee na walemavu hao.


HOTUBA YA MHESHIMIWA MAMA JANETH MAGUFULI, MKE WA RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA KWENYE KITUO CHA MAKAZI YA WAZEE NA WATU WALEMAVU WASIOJIWEZA
NUNGE, KIGAMBONI, TAREHE 3 FEBRUARI, 2016

Mheshimiwa Bibi Sophia Mjema, Mkuu wa Wilaya ya Temeke,

Ndugu Ojuku Mgedzi, Mkuu wa kituo cha Nunge,

Ndugu Viongozi mliopo hapa,

Wananunge wote,

Wageni waalikwa,

Mabibi na Mabwana.


Asalaam aleikhum, Bwana Yesu asifiwe, Tumsifu Yesu Kristo.
Awali ya yote napenda kuchukua nafasi hii kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutukutanisha mahali hapa leo hii tukiwa salama na afya njema. Aidha, napenda kuushukuru uongozi mzima wa kituo hiki kwa mapokezi mazuri kwangu mimi binafsi pamoja na ujumbe nilioambatana nao.
Naombeni mniruhusu pia kuchukua nafasi hii kuwasilisha kwenu salamu nyingi kutoka kwa Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Ameniomba niwaarifu kuwa yupo pamoja nanyi na kwamba Serikali itaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali katika kuhakikisha wazee na watu wasiojiweza wanapata huduma zote muhimu kwa kadri ya uwezo wake.

Wageni waalikwa,
Mabibi na Mabwana,
Bila shaka, sisi sote tuliopo mahali hapa tunatoka kwenye familia au maeneo yenye wazee au watu wenye ulemavu wasiojiweza. Aidha, sisi sote tunafahamu kuwa wazee na watu wasiojiweza wanahitaji upendo, kuthaminiwa na kusaidiwa. Mtakubaliana nami pia kuwa kipimo kimojawapo cha kupima jamii iliyostaarabika na inayoheshimu misingi ya utu ni kuangalia namna inavyowathamini wazee na watu wasiojiweza.
Jambo la kutia faraja ni kwamba, nchi yetu ni miongoni mwa nchi zinazothamini na kuwaheshimu sana wazee na watu wasiojiweza. Miongozo na sera mbalimbali zenye lengo la  kulinda na kutetea maslahi ya wazee na watu wasiojiweza zimeweza kupitishwa na Serikali, ikiwemo Sera ya Taifa ya Wazee na Sera ya Taifa ya Maendeleo na Huduma kwa Watu wa Wenye Ulemavu. Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi ya Mwaka 2015 imeeleza pia namna watu wa makundi maalum, wakiwemo wazee na walemavu, watakavyopewa kipaumbele. Kwa kuzingatia ilani hiyo, Mheshimiwa Rais katika muundo wa Serikali ameweka Wizara inayoshughulikia masuala ya walemavu. Uwepo wa kituo hiki cha Nunge na vituo vingine vingi kama hivi hapa nchini ni kiashiria kuwa nchi yetu inawaheshimu na kuwathamini sana wazee na watu walemavu wasiojiweza.
Wageni waalikwa,
Mabibi na Mabwana,
Nikiri kwa dhati kabisa mimi nikiwa ni Mke wa Rais, mama, mlezi na mwalimu nimefarijika sana kuwepo mahali hapa siku ya leo. Uwepo wangu mahali hapa umenipa fursa ya kubadilishana mawazo na watoa huduma na wahudumiwa kuhusu mafanikio na changamoto zinazowakabili pamoja na namna ya kuzitatua.
Napenda kuchukua nafasi hii kuwapongeza kwa dhati kabisa uongozi na watumishi wote wa kituo hiki na vituo vingine nchini kwa kazi kubwa mnayoifanya licha ya kukabiliwa na changamoto kadhaa. Napenda kuwahakikishia kuwa Watanzania wote tunatambua na kuthamini sana kujitoa kwenu katika kuwahudumia wazee na watu wasiojiweza.
Changamoto zenu nimezisikia na nawaahidi kuwa tutashirikiana na wadau wote kuzitafutia majibu yake. Hata hivyo, napenda kuchukua nafasi hii kuziomba na kuzihamasisha taasisi za Serikali na zisizo za Serikali kushirikiana katika kutatua changamoto zinazokabili kituo hiki na vingine vilivyopo katika maeneo mbalimbali nchini, ambavyo nimeambiwa idadi yake ni 17. Baadhi ya chamoto hizo ni pamoja na uchakavu wa miundombinu; uhaba wa rasilimali fedha na watu, pamoja na maslahi duni ya watoa huduma; upungufu wa vitendea kazi na huduma za jamii; pamoja na suala la uvamizi wa eneo la kituo.  Nimefarijika kwamba miongoni mwa wageni waliopo mahali hapa ni viongozi wa Serikali. Hivyo, ni matumaini yangu kuwa wamechukua changamoto zenu, hususan suala la uvamizi wa eneo hili la kituo, na kwamba watatafuta ufumbuzi.
Wageni waalikwa;
Mabibi na Mabwana,
Ni dhahiri kuwa Serikali ina wajibu mkubwa katika kuhudumia wazee na watu wasiojiweza. Hata hivyo, mtakubaliana nami kuwa Serikali pekee haiwezi kumaliza matatizo yote yanayowakabili wazee na watu wasiojiweza. Hivyo basi, sisi sote kwa pamoja tunao wajibu wa kusaidia nguvu za Serikali katika kuwahudumia wenzetu hawa. Na kwa kutambua hilo, mimi na wenzangu nilioambatana nao tumeamua kutoa zawadi yetu ndogo kwenu. Zawadi hiyo inajumuisha vitu vifuatavyo:
i.                     Mchele kilo 3000
ii.                   Unga kilo 3000
iii.                  Maharage kilo 1200.

Kulingana na idadi yenu niliyopewa  kila mmoja atapewa kilo 25 za mchele, kilo 25 za unga na kilo 10 za maharage.

Natambua zawadi tuliyoileta ni ndogo na haiwezi kumaliza matatizo yote mliyonayo. Lakini ni matumaini yangu kuwa zawadi hii inaweza kuwa chachu ya kuamsha hamasa ya kwa watu na vikundi vingine kujitoa kusaidia watu wasiojiweza. Ni imani yangu kuwa endapo watu wote tutajitoa kwa dhati tutaweza kuwahudumia wazee na watu wasiojiweza na hivyo kuwapunguzia makali ya maisha. Tukakumbuke ya kuwa ‘kutoa ni moyo ni si utajiri” na kwamba “sisi sote ni wazee na walemavu watarajiwa”.

Mheshimiwa Mkuu wa Wilaya
Mkuu wa kituo,
Mabibi na Mabwana,
Napenda kuhitimisha hotuba yangu fupi, kwa kutoa tena Shukrani zangu za dhati kwa uongozi wa Kituo kwa kunikaribisha vizuri mimi na wenzangu na pia kwa kazi kubwa mnayoifanya ya kuwahudumia wenzetu wenye shida mbalimbali. 

Asanteni kwa kunisikiliza.

No comments: