Social Icons

Saturday 5 August 2017

A.K.A SIO ISHU, ISHU NI UBORA WA KAZI!



Na Mohammed Hammie Rajab
A.K.A ni kirefu cha maneno ya kiengereza ambayo ni "Also known as", ikiwa na maana ya 'Pia nafahamika kama', ambapo mtu akitaka kujulikana ama kufahamika kwa jina jengine ambalo sio rasmi, huwa anatumia a.k.a kwa kiashirio cha jina mbadala.
Jina linapokuwa rasmi mara nyingi hutumika zaidi kwenye vitambulisho, vyeti, shuleni na hata maofisini kutokana na taratibu za kisheria zilizowekwa na serikali, huwezi kukuta mtu anatumia a.k.a kwenye masuala yanayotaka utaratibu.

Muziki wa Bongo Fleva umekuwa maarufu sana hapa nchi na hata nje, umaarufu wa muziki huu pia unachagizwa na majina ya wasanii wake ambapo tumeshuhudia wasanii wengi  wakitumia zaidi a.k.a pasipo majina yao halisi, japokuwa kuna wasanii wachache wanaotumia majina yao.
Alli Kiba na ndugu yake Abdul, ukiacha uhalisia wa majina yao ya kati ambapo wote wanatumia Salehe lakini utagundua fika kuwa hawakutengeneza a.k.a ili kupata majina yao ya kisanii, badala yake wametumia majina yao rasmi.
Wengine ni Banana Zorro na ndugu yake Maunda Zoro ambao hawakutumia muda kutengeneza a.k.a na bado wanafahamika, wapo pia wasanii ambao A.K.A zao zinashahabiana na majina yao halisi ambao ni Bernad Paul (Ben Paul), Jaffar Msham Ally (Jaffarai), Snura Mushi (Snura) na Ambwene Yesayah (AY) ambaye ameunganisha jina lake na ubini wake kupata A.K.A.
Kwa majina haya kidogo unaweza kusema afadhali kwa kuwa ni rahisi hata kuyatabiri, tofauti unaposikia jina kama Omari Faraji Nyembo halafu ukaambiwa kuwa ndio Ommy Dimpoz, au  Ibrahim Mussa ambaye ni ROMA, unaweza usielewe kidogo.
Wapo wasanii wengine pia ambao lazima ikuchukue muda kufahamu majina yao halisi, mfano ni Emmanuel Simwanga (Izzo B), Abdul-Aziz Abubakar Chende (Dogo Janja), Emmanuel Elibariki (Ney Wa Mitego), na hata Khery Sameer Rajab (Mr Blue), zaidi utaangua kicheko tu.
Hao ni wachache tu, lakini ukienda ndani zaidi utagundua kuna wimbi kubwa la wasanii wa Bongo Fleva wanaotumia zaidi a.k.a kiasi cha kupoteza majina yao halisi nchini tofauti na fani nyengine kama vile soka na filamu.
Tofauti kubwa iliyopo baina ya wasanii wa Bongo Flava na waliopo kwenye fani ya soka au filamu ni uwazi wa majina yao, mfano marehemu Steven Kanumba pamoja na kutumia a.k.a  ya the Great, lakini jina lake halisi lilikuwa likifahamika zaidi kuliko jina lake mbadala. Wengine ni Shamsa Ford, Jackline Wolper, na Yusufu Mlela ambao hata kama wana A.K.A lakini hazisikiki kama yalivyo majina yao halisi.
Japokuwa utakubaliana na mimi kuwa wapo baadhi ya wasanii wa filamu nchini ambao nao wamepoteza majina yao halisi na kutumia zaidi majina mbadala, mmoja wapo ni Elizabeth Michael (Lulu), Blandina Chagula (Johari), Mahsein Awadhi (Dokta Cheni), Single Mtambalike (Richie), na Vincent Kigosi ambaye anafahamika zaidi kama Ray.
Huwa najiuliza kuna tatizo gani mtu akabakia na jina lake halisi pasipo na kuwa na A.K.A, ikibidi alitumie hilo hata katika shughuli zake za kisanii ama fani yake?
Kwa mfano Diamond angepungua nini endapo angetumia jina lake la Naseeb katika muziki wake, au Ibrahim Mussa ambaye ni ROMA, mbona Banana Zorro ni msanii mkubwa na bado anafahamika sana kupitia jina lake halisi.
Nimekuwa nikifatilia sana wacheza filamu kutokea nchini Nigeria lakini nimegundua waigizaji wachache sana wanaotumia A.K.A, lakini waigizaji wakubwa kama Genevieve Nnaji, Rita Dominic, Omotola Jalade Ekeinde, na Ramsey Nouah hawana majina mbadala na badala yake wanatumia sana majina yao halisi na bado wanabamba.
Utumiaji wa majina mbadala (A.K.A) ni utashi wa mtu mwenyewe, hauna uhusiano wowote kuwa unapotumia jina mbadala ndio utafahamika zaidi katika jamii inayokuzunguka.
Kufahamika kwako kunatokana na ubora wa kazi unayoifanya, naamini kuwa hata kama Lulu angetumia jina lake halisi la Elizabeth Michael katika uigizaji bado angefahamika tu kutokana na ubora wa kazi yake, hivyo hivyo kwa Zuwena Mohamedi (Shilole)
Niseme tu A.K.A sio ishu, ishu ni kukomaa na ubora wa kazi unazofanya na watu watakujua kupitia ubora huo na sio A.K.A, wapo wenye A.K.A kali na bado hawafahamiki.
Makala Hii Imeandikwa na:
Mohammed Hammie Rajab
Phone: 0719000010

No comments: