Na Mohammed Hammie Rajab
A.K.A ni kirefu cha maneno ya kiengereza ambayo ni "Also known as",
ikiwa na maana ya 'Pia nafahamika kama', ambapo mtu akitaka kujulikana
ama kufahamika kwa jina jengine ambalo sio rasmi, huwa anatumia a.k.a
kwa kiashirio cha jina mbadala.
Jina linapokuwa rasmi mara nyingi hutumika zaidi kwenye vitambulisho,
vyeti, shuleni na hata maofisini kutokana na taratibu za kisheria
zilizowekwa na serikali, huwezi kukuta mtu anatumia a.k.a kwenye masuala
yanayotaka utaratibu.
Muziki wa Bongo Fleva umekuwa maarufu sana hapa nchi na hata nje,
umaarufu wa muziki huu pia unachagizwa na majina ya wasanii wake ambapo
tumeshuhudia wasanii wengi wakitumia zaidi a.k.a pasipo majina yao halisi, japokuwa kuna wasanii wachache wanaotumia majina yao.
Alli Kiba na ndugu yake Abdul, ukiacha uhalisia wa majina yao ya kati
ambapo wote wanatumia Salehe lakini utagundua fika kuwa hawakutengeneza
a.k.a ili kupata majina yao ya kisanii, badala yake wametumia majina yao
rasmi.
Wengine ni Banana Zorro na ndugu yake Maunda Zoro ambao hawakutumia muda
kutengeneza a.k.a na bado wanafahamika, wapo pia wasanii ambao A.K.A
zao zinashahabiana na majina yao halisi ambao ni Bernad Paul (Ben Paul),
Jaffar Msham Ally (Jaffarai), Snura Mushi (Snura) na Ambwene Yesayah
(AY) ambaye ameunganisha jina lake na ubini wake kupata A.K.A.
Kwa majina haya kidogo unaweza kusema afadhali kwa kuwa ni rahisi hata
kuyatabiri, tofauti unaposikia jina kama Omari Faraji Nyembo halafu
ukaambiwa kuwa ndio Ommy Dimpoz, au Ibrahim Mussa ambaye ni ROMA, unaweza usielewe kidogo.
Wapo wasanii wengine pia ambao lazima ikuchukue muda kufahamu majina yao
halisi, mfano ni Emmanuel Simwanga (Izzo B), Abdul-Aziz Abubakar Chende
(Dogo Janja), Emmanuel Elibariki (Ney Wa Mitego), na hata Khery Sameer
Rajab (Mr Blue), zaidi utaangua kicheko tu.
Hao ni wachache tu, lakini ukienda ndani zaidi utagundua kuna wimbi
kubwa la wasanii wa Bongo Fleva wanaotumia zaidi a.k.a kiasi cha
kupoteza majina yao halisi nchini tofauti na fani nyengine kama vile
soka na filamu.
Tofauti kubwa iliyopo baina ya wasanii wa Bongo Flava na waliopo kwenye
fani ya soka au filamu ni uwazi wa majina yao, mfano marehemu Steven
Kanumba pamoja na kutumia a.k.a ya the Great, lakini jina
lake halisi lilikuwa likifahamika zaidi kuliko jina lake mbadala.
Wengine ni Shamsa Ford, Jackline Wolper, na Yusufu Mlela ambao hata kama
wana A.K.A lakini hazisikiki kama yalivyo majina yao halisi.
Japokuwa utakubaliana na mimi kuwa wapo baadhi ya wasanii wa filamu
nchini ambao nao wamepoteza majina yao halisi na kutumia zaidi majina
mbadala, mmoja wapo ni Elizabeth Michael (Lulu), Blandina Chagula
(Johari), Mahsein Awadhi (Dokta Cheni), Single Mtambalike (Richie), na
Vincent Kigosi ambaye anafahamika zaidi kama Ray.
Huwa najiuliza kuna tatizo gani mtu akabakia na jina lake halisi pasipo
na kuwa na A.K.A, ikibidi alitumie hilo hata katika shughuli zake za
kisanii ama fani yake?
Kwa mfano Diamond angepungua nini endapo angetumia jina lake la Naseeb
katika muziki wake, au Ibrahim Mussa ambaye ni ROMA, mbona Banana Zorro
ni msanii mkubwa na bado anafahamika sana kupitia jina lake halisi.
Nimekuwa nikifatilia sana wacheza filamu kutokea nchini Nigeria lakini
nimegundua waigizaji wachache sana wanaotumia A.K.A, lakini waigizaji
wakubwa kama Genevieve Nnaji, Rita Dominic, Omotola Jalade Ekeinde, na
Ramsey Nouah hawana majina mbadala na badala yake wanatumia sana majina
yao halisi na bado wanabamba.
Utumiaji wa majina mbadala (A.K.A) ni utashi wa mtu mwenyewe, hauna
uhusiano wowote kuwa unapotumia jina mbadala ndio utafahamika zaidi
katika jamii inayokuzunguka.
Kufahamika kwako kunatokana na ubora wa kazi unayoifanya, naamini kuwa
hata kama Lulu angetumia jina lake halisi la Elizabeth Michael katika
uigizaji bado angefahamika tu kutokana na ubora wa kazi yake, hivyo
hivyo kwa Zuwena Mohamedi (Shilole)
Niseme tu A.K.A sio ishu, ishu ni kukomaa na ubora wa kazi unazofanya na
watu watakujua kupitia ubora huo na sio A.K.A, wapo wenye A.K.A kali na
bado hawafahamiki.
Makala Hii Imeandikwa na:
Mohammed Hammie Rajab
Email: ankomo25@yahoo.com
Phone: 0719000010
No comments:
Post a Comment